Tuesday 21 October 2014

UHALISIA WA MFUMO WA UONGOZI




Je twaelewa mfumo wa uongozi ulivyo katika kila taasisi nchini mwetu na je twajua chanzo cha kuwepo matabaka mbalimbali? Katika makala haya nimeangazia na kuyajibu maswali haya paruwanja kama yavyodhihika uongozini

Kenya imegawika katika matabaka walalahai na hawa ni walio na uwezo wa kukimu mahitaji yao ya kila siku na wenye uwezo wa kuishi maisha ambayo kila mja angependa au anatamani kuyaishi. Kundi la pili ni la walalahoi ambalo ndilo hasa linajumuisha asilimia kubwa zaidi nchini. Hili kukithi mahitaji yao ni kero kubwa sisemi ni ngumu. Hili ni kundi ambalo linapigania kile ambacho kilisalia baada ya kundi la awali kukinai. Hili ni dhahiri utembeapo katika sehemu za madongoporomoka pale hali ya maisha ni ya kubahatisha chambilecho wenyeji.

Kuna matabaka mengine mawili ambayo kwa kiasi kikubwa huchangia kuwepo kwa matabaka ya hapo awali. Kuna la  watawala na watawaliwa ama ukipata muda sema wapiga kura na wapigiwa kura. Haya mawili kwa maoni yangu ndiyo huamua hatma ya nchi yoyote ile. Kwanza kabisa wapiga kura ndio mhimili mkuu wa kudhibiti nchi. Nina uhakika kwamba baada ya makala haya msomaji na mpenzi na mkubali wa uhalisia atakubaliana nami. Wakati wa kampeini za kisiasa ndio kila hila ya kila aina huzinduliwa. Kila anayesimama jukwaani kutoa hotuba hudai kwamba atageuza sehemu au kitengo alichochaguliwa kuhudumu au kuwakilisha kuwa paradiso. Sisi tukiwa wapiga kura hushangilia na kuwapa sifa bila hata kujua kuwa ni chui kavalia ngozi ya kondoo chambilecho wazee wetu. Wanapoingia madarakani huzuka na sera madhubuti ambazo kwangu ni za kuwafumba wananchi wapiga kura macho. Pindi tu baada ya kutulia ofisini inakuwa ni mwamba ngoma huvuta upande wake. Unakuwa ni wakati wa kuvuvia viriba na kujenga makasri yote kwa hisani ya mali ya mpiga kura. Baada ya miaka mitano wanarudi hata bila zaibaki za usoni na kuomba kura nasi bila kufikiria tunawapa kura na kuwarejesha mamlakani. Tabia ya imeridhishwa tangu hapo jadi na waliotangulia.
  
Taswira hii ya uongozi na siasa si tofauti na vyuoni au uchaguzi na siasa katika vyuo vikuu. Imekuwa ni kawaida kuandaa midahalo ili kubaini ambacho viongozi wetu watatufanyia baada ya kutwaa uongozi.katika midahalo hii ubabe na matapo hushamiri kila mmoja akijaribu kumpiku mpinzani wake. Hapa sauti na jinsi utashughulikia maswala yaliyoulizwa ndio nguzo muhimu ya kushawishi wafuasi. Kinachokerekete maini ni kwamba mtindo ule ule wa maji hufuata mkondo huendelezwa. Tunaahidiwa paradise kumbe matokeo ni jehanamu chambilecho Muingereza. Unagundua waliochaguliwa wanawakilisha watu tofauti kabisa na waliowachagua na inakuwa kwanza ni kushulikia maswala yanayohusisha maisha yangu. Matokeo ya hayo ni kuwa na usimamizi kandamizi na minongono ya kila aina kwa ajili ya uongozi. Hii huathiri utendakazi wa chuo husika kwani ushirikiano haupo.

Nitakuwa mtovu wa taadhima nisipowashukuru na kuwapa mkono wa heko wanaoelewa kilichowapeleka ofisini. Hili ndilo kundi ambalo kwao masilahi ya watawaliwa hupewa kipaumbele. Ni jambo la kuajabia kwamba adinasi hawa ni adimu kama maziwa ya kuku ama kama tone jangwani.
Ili kupata nchi na chuo tunachotamani ni kwetu sisi watawaliwa kuketi na kujaribu kutafakari mustakabali wetu kuhusiana na viongozi ambao tunapanga kuchagua. Aidha nisionekane mwanaharakati au mwanamapinduzi bali ninachotaka kusema ni kwamba tuzitathmini sera ambazo viongozi wetu wanatuahidi na utekelezwaji wazo na tusiwe na dhana ya kisiasa na kikabila tunapopiga kura.
Kwa viongozi wetu nawapiga mijeledi kwa kuwasaliti wafadhili wao na kukosa kuwawajibikia.
  
Mwandishi: Samwel Mburu

No comments:

Post a Comment