Friday 24 October 2014

Hongera kiswahili.


Mimi kama kiumbe niliyebahatika kuzaliwa katika sayari hii, nimemeamua kukupa kongole ewe Malkia Kiswahili kwa sababu wewe ni shujaa. Licha ya madhila yote tumewahi kukufanyia sisi kama waja hapa duniani, wewe umekuwa mkarimu kwa kutufanyia fadhila nyingi ambazo sisi binadam hatukustahili machoni pako. Kwa hilo, pokea  shukran sufufu kutoka kwangu kwa niamba ya wapenzi wako wote duniani.

Naomba niguzie zile njia umeonyesha ukakamavu na ushujaa wa hali ya juu kwa kustahimili mawimbi makali na tufani zinazotokea katika bahari hii ya maisha. Wengi wamejaribu kwa udi na uvumba kukunyang`anya kizazi cha bala lako afrika. Mahali ambapo wewe ulizaliwa na ukafaham kuwa nyumbani. Niliona wakikunyanganya hata watoto wadogo kwe  shule ya chekechekea. Niliona wakipokea mijeledi mikali kwa sababu ya kukuhusudu na kukuenzi, lakini ulifika na kuwafariji kwa mishororo ya kuliwaza nyoyo zao zilizo umia. Na kwa wale hawakukufa moyo, nawaona mahali uliwafikisha ewe Kiswahili. 

Wengine wamepokea hadhi kubwa sana duniani. Sina haja ya kuwataja majina kwa sababu unawajua  bayana ila niseme hao ni wanao kindakindaki. Wapo wale wakereketwa wa kukutaftia mahali pako katika jamii. Bila  kumsahau Yule mwanao Usadh Wala bin Wala. Si unajua mpaka ameanzisha Chuo cha Wasta? 
 Chuo ambacho kinaeneza kila mbinu muhimu ya kukupatia wana wengi wa afrika na jirani zake.

Nimeona ukiwashukuru wanao na wapenzi kindakindaki. Mimi kwanza ulifanya nikaja chuo kikuu sasa nami ni mwana mlimani! Wengine umewatunuku nafasi ya kupaa juu angani mpaka ng`ambo ya maji. Wengine uliwapa ajira na ukawapa shukran sufufu kwa kuinua kipato chao.

Hongera kwa kustahimili mawindo ya wale wanao kuwinda ili wakuangamize. Hawa ni wale wanaowadharau wanao wanaokuenzi kindakindaki wakisema wanaozungumza Kiswahili wana hadhi ya chini. Wengine wamo mbioni kueneza kasumba kwamba Kiswahili ni kigumu, Vipi na tangu lini mwana wa mji akaita mgeni Baba? Ama kweli wamewachanganya baadhi ya wanao. Licha ya hayo nimekuona ukiwatuma wajumbe wako kukutetea katika mijadala yetu na hata ya kimataifa. Kwa kweli wewe ni mwerevu hakika.

Nimeona kiamboni wengine wamekuja na lugha zingine ili wakutoe katika ramani ya dunia. Wameleta sheng`  ili wakunyang`anye hadhira kwa wana wa miji na vijiji. Jambo moja limenishangaza, ni jinsi ambavyo wewe unaendelea kusambaa kote duniani. Nimewaona wanao wakipeleka ujumbe wako mbali na nyumbani ugaibuni. Marekani, China, Ulaya wote wako mbioni kusoma sheria na kaida zako ili wawe na nafasi katika karne hii ya utandawazi. Nimekuona umepenya mpaka ndani ya technologia. Nina furaha kwa sababu niliyaona makao yako kwenye mtandao. Bila shaka hutakufa kipenzi changu Kiswahili. Sasa kamusi nyingi nimeziona zinazokuangazia wewe, na hata katika katiba ya Kenya wewe ulijioatia nafasi yako madhubiti katika dola hili.

Afrika yote inakukumbatia tena kwa hamu. Kuna jambo ambalo nimeliona ukilifanya lakini bado halijatimia. Sio lazima niwe nabii lakini ninauwezo wa kusema hivi karibuni utakuwa wa kutumika Afrika nzima. Nimewaona wakitafuta lugha moja ya kuwaunganisha  wana Afrika na alama zako ziko kidedea kuliko lugha za  Fulani, Yoruba, Mande na Hausa ambazo zilipigiwa kura kujitoza ulingoni kukabiliana nawe. Lakini linalo nipa tabasamu, ni kwamba wewe bado uko mbali na wenzio kwa sababu ya historia yako ndefu na machapisho kadha wa kadha. Pili usuli wako ni wa kibantu na lugha nyingi Afrika ni za kibantu na ndio maana ikilinganishwa na wenzako, wewe una wasemaji wengi. Ndio maana wasomi kama Wole Soyinka, Mohammed  Hasan Abdulaziz na wengine walipokutana mjini Lagos Mwaka wa 1976, walikupigia  kura na hakika hiyo siku itafika kipenzi changu na utafikwa koja.

Ombi langu kuu kwako ni kwamba endelea kuzidi kung`ang`ana na hatimaye utafanikiwa. Ndio najua una shida kidogo kidogo kama za misamiati mingi tu ya kueleza mambo mengi ya kisayanzi na kiteknologia lakini usife moyo kwani wenzako pia wamekopa. Hata wewe una uhuru wa kukopa. Licha ya hayo watie wanao shime ili wasichoke katika utafiti kila siku na kuleta misamiati kwa sababu wewe unakua kwa njia moja kubwa sana.

Nakuomba uzidi kuwakumbusha wale wanao eneza dhana potovu kwamba wewe ni wa haiba ya chini ukiwapa mifano ya wanao wengi ambao wameendelea sana kimaisha kupitia kukukumbatia  wewe. Nangoja kuona siku ile utatumika kama nembo ya kutambulisha Afrika na dunia kwa jumla. Hakika hongera kipenzi changu  kwa juhudi kubwa ulizonazo kwa kuwafaidi wanadam na njia mufidi ya kuwasiliana. Mungu azidi kuwabariki wana na wapenzi wako duniani. 

Mwandishi: Franklin Momanyi.  Mwanafunzi Chuo Kikuu cha Chuka. 


No comments:

Post a Comment