Sunday 19 October 2014

TUTUMIE TULICHO NACHO KUPATA AJIRA




Wakati wa ukoloni mwafrika hakuruhusiwa kumiliki kitu chochote ambacho kilidhaniwa kuleta mapato. Hali hii iliendelea hadi pale uhuru ulipatikana ndiposa umilisi wa kitu kwa upande wa mwafrika ukawa. Mtu alipopapata kazi ofisini ilikuwa ni fahari kubwa sana na alitarajia kuheshimika sana. Pindi baada ya uhuru nchi nyingi zilijitawala ikiwemo nchi yetu na wakati huo nafasi za kazi serikalini na hata makampuni ya kibinafsi zikawa nyingi kutokana na utengenezaji wa bidhaa muhimu. Watu walifurahia hali ya maisha kwani kila mja aliweza kuyakidhi mahitaji yake. Faida nyingi naweza nikazitaja hadi nibakie kuandika riwaya.
Hiyo ni historia wala haiwezi ikajiradidi. Kutokana na kero la ufisadi  nafasi za kazi zimewa finyu kwani asiye na kitu cha kupeana au kutokuwa na nasaba na wakubwa hapati kazi. Hali hii imesababisha hali ya maisha kuwa ghali mno. Fauka ya hayo imepelekea baadhi ya makampuni na taasisi za uundaji kupata hasara kutokana na kuwaajili watu ambao hawajahitima ambao wakiulizwa hawaungami. Utasikia vijana wengi ambao wamehitimu masomoni wengi wao wakiwa wa vyuo vikuu wakilia hamna. Hao ndio utawaona wakati wote wakipiga gumzo zisizo na manufaa yoyote maishani. Haya hamna yeyote anayepinga wala kukataa kuwa hakuna kazi. Jambo hili li wazi kama meno ya ngiri chambilecho watangulizi wetu.. swali langu ni je iwapo ulipitia shule ya msingi, upili na hatimaye chuo kikuu ni nini ambacho huwezi ukafanya ili kujipa riziki? Tatizo letu kubwa limewa kutegemea tu kazi ya ofisi hasa wale ambao wamehitimu vyema masomoni. Uzembe na ukosefu wa kuwa wabunifu kumezidi kuharibu hali ya maisha.
Ni jambo la busara na mwafaka sana kuwa na maono ila kuna dhana potovu ambayo walohitimu au wanaopania kuhitimu kuwa pasipo kufanya kazi ofisini kazi nyingine zozote si kazi. Kwa kweli tumezungukwa na nafasi nyingi tu za kazi ila tu hatutaki kuzitumia kwa hofu ya kusemwa kuwa walihitimu ila hawafanyi kazi ya viwango vyao. Tusione kana kwamba waliosema kuwa waja ni ngamba hawakosi la kuamba walikosea. Waache wawe vidudumtu na waeneza umbeya lakini mwisho wa siku watalala. Ufaulu ama usifaulu lazima binadamu ataongea hivyo tusiogope kusemwa kwa chochote tukifanyacho. Upo wakati ambao tutahitajika kufanya mambo yaliyo chini ya viwango vyetu ili kukidhi mahitaji yetu wala tusione haya ama aibu kuyachangamkia. Ukweli na ukweli uchi uliopo ni kwamba nafasi za ajira ni finyu sana hivyo twafaa kujitengenezea nafasi za kazi. Utagundua kuwa mamantilie wengi wamehitimu ila hawaogopi kusemwa kwa kazi wafanyazo.
Nawarai wanaohitimu kuwa tusitegemee kuajiriwa ila tupanie kubuni nafasi za kazi.ili kukimu mahitaji yetu ya kila siku. Tutupilie mbali dhana ya kwamba lazima tuajiriwe. Nchi nyingi ambazo zimeendelea imekuwa ni juhudi kutoka kwa wanaanchi za kujituma na kuelewa kuwa maisha ni yao hivyo kutegemea kuajiriwa itakuwa ni kama kualika taabu na matatizo kwako.
Nikihitimisha nasema kwamba kazi ni kazi na  mchagua jembe si mkulima kwamba  mtegemea cha nduguye hufa maskini aidha changu hata kiwe kibovu ni bora kuliko chetu. Tutumie maarifa tuliyopata maishani kujipa ajira.
Kauli yangu ni kuwa, Katu sitachagua wala kubagua kazi yoyote mradi tu yanipa riziki.

Mwandishi: Samwel Mburu

No comments:

Post a Comment